Our Lady of Medjugorje Messages

Wanangu wapendwa! Kwa upendo wa kimama nataka kuwafundisha uadilifu, natamani kwamba katika kutenda kwenu kazi kama mitume wangu muwe wenye haki, maamuzi na hasa waadilifu. Natamani kwamba, kwa neema ya Mungu, muweze kupokea Baraka ya Mungu. Natamani, kwa njia ya kufunga na kusali, muweze kupata kutoka kwa Baba wa Mbinguni ujuzi, uhalali, utakatifu wa kimungu. Kwa ulinzi wa Mwanangu na wangu mtakuwa mitume wangu, ambao wanaweza kueneza neno la Mungu kwa wote wasiolijua, na mtaweza kushinda mapingamizi mtakayokutana nayo njiani. Wanangu, kwa njia ya baraka neema itawashukia, nanyi mtaweza kuilinda neema hiyo kwa kufunga na kusali, kwa kujitakasa na kujipatanisha. Mtakuwa na utendaji fanisi ninaohitaji kutoka kwenu. Waombeeni wachungaji wenu ili mionzi ya neema ya Mungu iangaze njia yao. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Salini, salini, salini ili mionzi ya sala yenu iwaguse watu wote mnaokutana nao. Wekeni Biblia Takatifu mahali pa kuonekana katika familia zenu, mkaisome ili maneno ya amani yatiririke ndani ya mioyo yenu. Nasali pamoja nanyi na kwa ajili yenu, wanangu, ili siku hata siku mzidi kuyapokea mapenzi ya Mungu. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa! Ili mpate kuwa mitume wangu na kuweza kusaidia wale walioko katika giza, ili waweze kuujua mwanga wa upendo wa Mwanangu, mnapaswa kuwa na moyo safi na mnyenyekevu. Hamwezi kusaidia ili Mwanangu azaliwe na kutawala mioyoni mwa wale wasiomjua, iwapo Yeye hatawali moyoni mwenu. Mimi nipo pamoja nanyi, natembea pamoja nanyi kama mama, nabisha hodi katika moyo wenu, usioweza kufunguka bila ya kuwa mnyenyekevu. Mimi nasali, lakini salini nanyi pia, wanangu wapendwa, ili muweze kumfungulia Mwanangu moyo wenu safi na mnyenyekevu na hivyo kuweza kupokea vipaji nilivyowaahidi. Hapo ndipo mtakapoongozwa kwa upendo na nguvu za Mwanangu, hapo ndipo mtakuwa mitume wangu, ambao wanaweza kueneza kwa walio karibu yao matunda ya upendo wa Mungu. Kutokana na ninyi na kwa njia yenu Mwanangu atafanya kazi, maana mtakuwa na Yeye kitu kimoja. Moyo wangu wa kimama unatamani muungano wa wanangu wote, kwa njia ya Mwanangu. Kwa upendo mkuu nawabariki na kuwaombea wateule wa Mwanangu, wachungaji wenu, Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Ninawaletea Mfalme wa amani ili Yeye awapatie amani Yake. Ninyi, wanangu, salini, salini, salini. Matunda ya sala yatajionyesha kwenye nyuso za watu waliojitoa kwa Mungu na Ufalme wake. Mimi pamoja na mwanangu Yesu tunawabariki nyote kwa baraka ya amani. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa, kwa upendo wa kimama na uvumilivu wa kimama naona kutangatanga kwenu na kuendelea kupotea kwenu. Kwa sababu hiyo mimi nipo pamoja nanyi. Nataka kwanza kabisa kuwasaidieni kupata kujijua ninyi wenyewe, ili baadaye muweze kuelewa na kutambua yote yanayowazuia kujua bila unafiki na kwa moyo wote upendo wa Baba wa Mbinguni. Wanangu, Baba hujulikana kwa njia ya msalaba: kwa hiyo msikatae msalaba: kwa msaada wangu, mkafanye bidii kuuelewa na kuupokea. Mtakapoweza kuupokea msalaba, mtaelewa pia upendo wa Baba wa Mbinguni. Mtatembea pamoja na Mwanangu na mimi. Mtajipambanua na wale ambao hawakujua upendo wa Baba wa Mbinguni, kujitofautisha na wale wanaomsikiliza lakini hawamwelewi, na wale wasioenda pamoja naye, na wasiomjua. Mimi nataka ninyi mjue ukweli wa Mwanangu na muwe mitume wangu; ili, kama wana wa Mungu, muwe na mawazo yaliyo juu ya mawazo ya kibinadamu na siku zote na katika yote mkatafute kila mara mawazo ya Mungu. Wanangu, salini na fungeni ili muweze kuelewa yote ninayowaombeni. Muombee wachungaji wenu mkatamani kujua, mkishirikiana nao, upendo wa Baba wa Mbinguni. Nawashukuruni.
Wanangu wapendwa! Leo nawaalikeni nyote kusali. Fungueni kwa kina mlango wa mioyo yenu, enyi wanangu, kwa sala, sala ya moyo na hivyo Yeye Aliye Juu ataweza kufanya kazi katika uhuru wenu na kuanzisha uongofu wenu. Hivyo imani yenu itakuwa imara kiasi cha kuweza kusema kwa moyo wenu wote: "Mungu wangu na yote yangu". Halafu mtaweza kuelewa, wanangu, ya kuwa duniani hapa yote hupita. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa, kwa moyo wa kimama nawaalikeni tena kupenda, kusali bila kukata tamaa kwa zawadi ya upendo, kumpenda Baba wa Mbinguni zaidi ya yote. Mtakapompenda Yeye, mtajipenda wenyewe na jirani zenu. Mambo hayo hayawezi kutengana. Baba wa Mbinguni yumo katika kila mtu, hupenda kila mtu na kumwita kila mtu kwa jina lake. Kwa hiyo, wanangu, kwa njia ya kusali sikilizeni atakalo Baba wa Mbinguni. Ongeeni na Yeye. Muwe na uhusiano wa binafsi pamoja na Baba, atakayeufanya mkubwa zaidi uhusiano wake nanyi, jumuhiya ya wanangu, mitume wangu. Kama Mama napenda kwamba, kwa njia ya upendo kumwelekea Baba wa Mbinguni, inukeni juu ya ubatili wa malimwengu na muwasaidie wengine kujua na kumjongea polepole Baba wa Mbinguni. Wanangu, salini, salini, salini kwa zawadi ya upendo, kwa sababu upendo ndiye Mwanangu. Muwaombee wachungaji wenu, ili wawapende ninyi siku zote, kama vile Mwanangu alivyowapenda ninyi na kuonyesha akitoa maisha yake kwa wokovu wenu. Nawashukuruni.
Wanangu wapendwa! Leo nawaalikeni mjifungulie kwa sali. Sala itasababisha miujiza ndani yenu na kwa njia yenu. Kwa hiyo, enyi wanangu, kwa moyo mkunjufu mtafuteni Yeye Aliye Juu ili awapeni nguvu ya kuwa wana wa Mungu, na yule Shetani asiwatikiseni kama matawi yatikiswavyo na upepo. Kateni shauri tena, wanangu, kwa Mungu na tafuteni tu mapenzi yake, hapo mtapata furaha na amani. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
Wanangu wapendwa! nawapendeni kwa upendo wa kimama, na kwa subira ya kimama nangojea upendo wenu na ushirikiano wenu. Nasali ili muwe jumuiya ya wana wa Mungu na wanangu. Nasali ili muweze kuwa jumuiya inayojihuisha kwa furaha na imani na upendo wa Mwanangu. Wanangu, nawakusanya kama mitume wangu na nitawafundisha jinsi ya kuwajulisha wengine upendo wa Mwanangu, na jinsi ya kuwafikishia habari njema, ambaye ni Mwanangu. Nipeni mioyo yenu iliyo wazi na iliyosafishwa, nami nitaijaza upendo wa Mwanangu. Upendo wake utaipa maisha yenu maana nami nitatembea pamoja nanyi. Nitakuwa pamoja nanyi hata tumfikie Baba wa Mbinguni. Wanangu, wataokoka tu wale ambao watatembea kwa upendo na imani kumwelekea Baba wa Mbinguni. Msiogope, nipo pamoja nanyi! Muwaamini wachungaji wenu kama Mwanangu alivyowaamini wakati alipowachagua, na muwaombee ili waweze kupata nguvu na upendo wa kuwaongozeni. Nawashukuruni.
Wanangu wapendwa! Leo pia nawaalikeni kusali. Uhusiano wenu na kusali uwe wa kila siku. Sala inasababisha miujiza ndani yenu na kwa njia yenu, na kwa hiyo, enyi wanangu, sala basi iwe ni furaha yenu. Hivyo uhusiano wenu na maisha utakuwa wa kina na wazi zaidi, pia mtaelewa kwamba maisha ni zawadi kwa kila mmoja wenu. Asanteni kwa kuitikia mwaliko wangu.
   




To compare Medjugorje messages with another language versions choose
<<Previous  1 ... 20 21 22 Next>>
Medjugorje WebSite